Thursday, October 6, 2011

Moto wateketeza ofisi za Star Times

Na Elisha Magolanga

Uchaguzi Igunga waigawa tena CCM

Na Moses Mabula, Tabora

SIKU tatu baada ya CCM kushinda uchaguzi wa Jimbo la Igunga, Mwenyekiti wa Chama hicho
mkoani Tabora, Bw. Hassan Wakasuvi ametoa siri ya wana-CCM wenzake wanaodaiwa wafuasi wa aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Bw. Rostam Aziz na swaiba wake, Bw. Edward Lowassa kuwa walitaka chama hicho kishindwe ili 'waheshimiane'.

Bw. Wakasuvi alitoa maneno hayo makali yaliyoambatana na vijembe, wakati akihutubia wana-CCM waliojikeza katika sherehe za kujipongeza kwa ushindi katika uchaguzi mdogo wa Igunga uliofanyika Oktoba 2, mwaka huu.

Katika uchaguzi huo, Bw. Dalali Kafumu wa CCM alishinda kiti hicho cha ubunge na hivyo kuchukua nafasi iliyoachwa wazi na Bw. Aziz.

Bw. Rostam alijiuzulu nyazifa zake zote za uongozi ndani ya CCM ukiwemo ubunge na ujumbe wa NEC Julai 14, 2011 kwa kile alichoita 'kuchoshwa na siasa uchwara', chuki na
kufitiniana miongoni mwa viongozi na wanachama.

Lakini kinyume na matarajio ya wengi, Bw. Aziz aliibuka kwenye uzinduzi wa kampeni na kuwaomba wakazi wa Igunga kumchagua mgombea wa CCM.

Katika hotuba yake hiyo, Bw. Wakasuvi alitumia muda mwingi kurusha vijembe na tambo, akisema, licha ya kwamba kulikuwepo na upinzani mkali kutoka nje ya chama na hata ndani ya
chama chake, kazi aliyoifanya inastahili kupongezwa na kwamba ushindi huo bila yeye CCM ingeambulia patupu.

“Najua wapo hapa miongoni mwetu ambao walitaka CCM ishindwe, hao nawapa pole na waende kliniki wakazae, maana tumeshinda. Lakini pia wapo waliotamani tupate ushindi hao nawapongeza na waendelee kushangilia, tumeshinda,” alisema Bw. Wakasuvi

“Watu hao walikuwa wakisema ni bora jimbo la Igunga tushindwe ili eti tuheshimiane, sasa tumeshinda naomba tuheshimiane” alisema.

“Mimi ndio nilikuwa mkuu wa majeshi huko Igunga, hakuna wakubisha, mimi ndo nilikuwa komandoo na nilikuwa naongoza mashambulizi dhidi ya wapinzani wetu kutoka ndani ya
CCM na wale kutoka vyama vya upinzani,” alitamba Bw. Wakasuvi.

“Kama ushindi tumepata ila najua wapo mliochukia pia najua mpo nyie mliofurahi, endeleeni kufarahia ili hawa waliochukia ikiwezekana wajinyonge," alisema Mwenyekiti huyo.

Utetezi kwa Mbunge Rage

Mwenyekiti huyo alivigeukia vyombo vya habari kwa kuvishambulia kwamba vilikuwa vinapendelea upande mmoja wa upinzani kutangaza taarifa za kampeni jimboni Igunga huku akimtetea mbunge wa Tabora Mjini, Bw. Ismail Rage kupanda jukwaani na bastola.

Bw. Wakasuvi alisema kuwa haoni tatizo la mbunge wake kupanda jukwaani na silaha kwa madai kuwa hali iliyokuwa Igunga mbunge wake alikuwa sahihi, na kwamba waandishi wa habari ndio waliolikuza suala hilo baada ya kuliripoti kwenye magazeti, lakini ni jambo la kawaida.

“Mimi mbona nilikuwa nayo kiunoni lakini hamkiniandika, nadhani mna chuki zenu na Rage nyie wanahabari,” alisema.

Bw. Wakasuvi anayeaminika kutoka kundi la Bw. Samuel Sitta ilielezwa kuwa katika kikao cha Kamati ya Siasa mkoa wa Tabora kilichofanyika wilayani Igunga kabla ya kuanza
kwa mchakato wa kampeni za uchaguzi huo, alimtuhumu Bw. Rostam na baadhi ya wafuasi wake kwa kusema, “hata kama mliomo humu ndani ya kikao mmenuna, hiyo ni shauri yenu,
CCM itashinda tu, kauli iliyoungwa mkono na mbunge wa Tabora mjini Bw. Aden Rage

Alisema “Hata kama Rostam ana pesa, hawezi kuwa maarufu kama CCM, hapa tutashinda uchaguzi hata bila yeye kuwepo," alikaririwa na waliohudhuria kikao hicho.

Alisema kwamba CCM ingeshinda uchaguzi kwa gharama yoyote ile kwa kuwa kina dola, kauli ambayo iliwakera baadhi ya waliohudhuria kikao hicho, na kumtaka arekebishe kauli yake kwamba kilichokuwa kinahitajika kwa sasa ni kuunganisha nguvu badala ya ubinafsi.

Katika kikao hicho kilichohudhuriwa pia na aliyekuwa Mratibu wa Kampeni za CCM, Bw. Nchemba, ilielezwa kuwa zaidi ya sh. milioni 800 zinahitajika ili kupata ushindi katika uchaguzi huo.

Wengine waliohudhuria mkutano huo ni Makamu Mwenyekiti wa CCM (bara), Bw. Pius Msekwa, mbunge Viti Maalum Bi. Munde Tambwe ambaye pia ni mjumbe NEC na Bw. Rage.

Mpashaji wa habari hizo, alilieleza gazeti hili kuwa Bw. Wakasuvi aliwaeleza wajumbe wa kikao hicho kuwa Bw. Aziz ameshindwa kuwaletea maendeleo wakazi wa jimbo la Igunga tangu
achaguliwe kushika nafasi hiyo mwaka 1994 baada ya kifo cha aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, marehemu Charles Kabeho.

Habari kutoka ndani ya chama hicho mkoani hapa zinabainisha kuwa Bw. Wakasuvi haelewani na baadhi ya viongozi wenzake ndani ya CCM mkoa na wilaya kutokana na kile kilichoelezwa ni miongoni mwa waasisi wa chama cha CCJ, yeye na Bw. Sitta.

Hata hivyo, alipoulizwa kuhusu madai hayo na maelezo yake mkutanoni, Bw. Wakasuvi alikanusha huku akiuliza, “wewe umezipata wapi habari hizi wakati kwenye mkutano haukuwemo